Get Paid To Promote, Get Paid To Popup, Get Paid Display Banner

Mamia wafurika maonesho ya Butiama

MAMIA ya watu wameendelea kujitokeza kijijini Butiama kwenye maonesho ya shughuli za idara mbalimbali zilizo chini ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, huku wengi wakisifu uamuzi wake wa kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara kijijini hapo.

Tangu maadhimisho hayo yazinduliwe wiki hii, mabanda ya taasisi mbalimbali ikiwemo Kampuni ya Tanzania Standard Newspapers (TSN) wachapishaji wa magazeti ya HabariLeo, HabariLeo Jumapili, Daily News na Sunday News yamekuwa yakifurika watu kutoka sehemu mbalimbali za Mkoa wa Mara.

Wakizungumzia maonyesho hayo, wanakijiji walisema wizara imetumia busara kuadhimisha siku hiyo katika eneo hilo ambalo ni chimbuko la Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere aliyefariki Oktoba 14, 1999.

Mdogo wake Mwalimu Nyerere, Jackton Nyerere (80), akiwa katika banda la Idara ya Habari, MAELEZO, alieleza kufurahishwa na picha mbalimbali za maktaba zinazomwonesha Mwalimu katika matukio tofauti.

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Habari, Maelezo, Raphael Hokororo alisisitiza kuwa zaidi ya watu 300 waliotembelea banda hilo tangu maonesho yaanze, wameipongeza idara hiyo kwa kuwa na maktaba ya picha za matukio mbalimbali ya miaka iliyopita.

Akizungumzia mafanikio ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania Bara, Hokororo alisema taasisi hiyo imefanikiwa kuwa kiunganishi kikubwa cha Serikali na wananchi. Pia ni kiunganishi cha Serikali na vyombo vya habari hususan vya binafsi.

Kuhusu changamoto zinazoikabili Idara hiyo, alisema ni kwa upande wa utunzaji wa kumbukumbu ambapo alisema ipo haja liwepo fungu la kutosha kuwezesha uwepo wa vifaa vya kisasa vya kuhifadhia kumbukumbu katika taasisi mbalimbali ili kuwezesha kizazi kijacho kuelewa historia ya nchi.

Alishauri pia mafunzo yatolewe juu ya mbinu za kisasa za kuhifadhi kumbukumbu isaidie kuongeza rasilimali watu.

Kwa upande wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Meneja Matangazo ya Studio na ya Nje, Julius Lucas alisema miongoni mwa mambo ambayo watu wengi wanaotembelea banda lao wanapenda kufahamu ni juu ya mabadiliko kutoka teknolojia ya analojia kwenda digitali.

Akizungumzia changamoto zinazolikabili shirika hilo, Mwandaaji Vipindi Mwandamizi, Martha Swai alisema wanalo jukumu kubwa la kuhakikisha kila Mtanzania anapata matangazo yao.

Alisema hawajamudu kumfikia kila Mtanzania jambo ambalo wanalifanyia kazi. Wakati huo huo, wajasiriamali kijijini Butiama wameeleza kufurahishwa na kuwepo kwa maonesho hayo wakisema yamesaidia kuwaongezea kipato kutokana na biashara ndogo ndogo.