Get Paid To Promote, Get Paid To Popup, Get Paid Display Banner

"AUNT SUZY" ANUSURIKA KUUAWA

BAADA ya shoga maarufu jijini Dar es Salaam, Ibrahimu Mohamed ‘Anti Suzy’ (25), kutoboa siri kwenye vyombo vya habari jinsi watoto wa kiume wanavyoharibiwa na wanaume na kueleza namna alivyobwagiwa mtoto wa mwaka amtunze, mwanamume aliyembwagia mtoto ameibuka na kumjeruhi kwa visu akitaka kumuua.

Mwanamume huyo (jina tunalo) mwenye mke, awali alikuwa akiishi na Anti Suzy kama mume na mke eneo la Jangwani, baada ya kumkimbia mkewe na alikorofishana na shoga huyo baada ya kumfanyia fujo na kumuibia.

 ‘Anti Suzy’ aliyejitangaza kuwa ni muathirika wa Virusi Vya Ukimwi kwa zaidi ya miaka 10 sasa, alisema mwanamume huyo alikuwa akimsumbua warudiane, lakini yeye alikataa na kumtaka aishi na mkewe na kutunza watoto badala ya kumng’ang’ania.

“Nilimwambia simtaki, vituko alivyonifanyia ukiacha kuniletea mtoto wa mwaka na nusu wa kike nimlee hapa nyumbani, alikuwa akinipiga, kunitukana na aliniibia vitu vyangu vyote. Kwanza nilishamwambia nimeathirika na Ukimwi ananifuata nini?” Alihoji shoga huyo.

“Jana (juzi) alinipigia simu akinitaka turidiane nikamwambia asinifuate kwanza nimeshaenda kwenye vyombo vya habari.”

Alisema alimwambia hivyo ili asimfuate, lakini baada ya kumweleza hayo, alimvamia nyumbani juzi kati ya saa nne na tano asubuhi akiwa na panga na visu akimtishia kumuua kama hawatarudiana na kama ataendelea kwenda kwenye vyombo vya habari kumuanika mambo yake.

“Nilikimbilia ndani na yeye akanifuata humo, akarusha panga anikate shingoni huku akisema ataniua, nikakwepa, lakini likanijeruhi shingo, kama haitoshi akachukua kisu alichokuwa nacho akanikata vidole.

“Damu ikaanza kutoka nyingi, alivyoona hivyo akanikaba kooni ili aninyonge, majirani waliposikia nakoroma, wakavunja mlango na kuniokoa,” alidai Anti Suzy.

Shoga huyo aliyeanza vitendo hivyo akiwa mkoani Mwanza, alisema aliamua yeye na mama mwenye nyumba kwenda Kituo Kidogo cha Polisi Jangwani kutoa taarifa na kupewa hati yenye namba MS/RB/10695/2011.

Alisema baada ya kwenda Polisi, aliandika maelezo na kutoa vielelezo likiwemo panga na kisu alivyovitumia kumjeruhi na aliandikiwa hati ya matibabu (PF3) na kwenda Hospitali ya Mnazi Mmoja kwa matibabu.

Polisi katika Kituo cha Jangwani walithibitisha kutokea kwa tukio hilo, lakini walisema mlalamikaji alijitaja kwa jina la kike ambalo ni Suzana Mohamed na tayari taarifa za suala hilo zimepelekwa Kituo cha Polisi Msimbazi kwa hatua za juu zaidi. Mkuu wa Kituo cha Msimbazi hakuwa tayari kutoa taarifa kuhusu suala hilo.

Aidha, Muuguzi aliyekuwa zamu juzi katika Hospitali ya Mnazi Mmoja ambaye hakupenda kutaja jina gazetini, pia alithibitisha kumhudumia mgonjwa, Suzana Mohamed (25) mkazi wa Jangwani aliyejeruhiwa shingo na vidole kwa kukatwa na visu akiwa na PF3.

Mama mwenye nyumba anakoishi ‘Anti Suzy,’ Manju Machu maarufu kama Bi Manju, alithibitisha jana kutokea kwa tafrani hiyo iliyosababisha mpangaji wake huyo akimbie kunusuru maisha yake.

“Alikuja hapa huyo mwanamume akamvamia akitaka kumuua, alikuwa na panga na kisu, tuliingilia maana alikuwa anasema lazima amuue, nikasema akimuulia hapa kwangu na mimi nitakuwa matatani, na nchi hii ina sheria, kama una kosa na mtu polisi si ipo? Sisi tulimpeleka huyu Polisi kutoa taarifa” alisema Machu.

Majirani wa Mohamed ‘Anti Suzy’ nao walithibitisha jana kushuhudia vurugu hizo na kumshauri shoga huyo kurudi kwao Mwanza ikiwa vitisho vitaendelea.

Mwishoni mwa wiki iliyopita, Mohamed alifanya mahojiano na gazetini na kueleza namna vigogo aliowataja kwa jina la mapedejee wanavyowatumia wao kwa gharama yoyote, wawatafutie watoto wadogo walioko shuleni na mitaani akiwataka wazazi, serikali na jamii kuwa macho na watoto hasa wa kiume.

Aidha, pia aliwaonya wanaume wasimfuate kwa kuwa yeye ni mwathirika wa Ukimwi na kwamba mashoga kama yeye wameathirika na ugonjwa huo. Usikose makala maalumu ya mahojiano ya ana kwa ana baina ya gazeti hili na Mohamed “Anti Suzy” katika gazeti hili keshokutwa Jumatano.